TRANSLATE THIS BLOG

Friday, September 7, 2012

TOKA TFF: TAIFA STARS v UGANDA CHAN 2014


TFF_LOGO.png

Release No. 142

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Septemba 7, 2012

MECHI YA NGAO YA JAMII KUCHANGIA HOSPITALI YA TEMEKE

Asilimia tano ya mapato yatakayopatikana kwenye mechi ya Ngao ya Jamii (Community Shield) kati ya Simba na Azam yatakwenda kwenye Hospitali ya Temeke mkoani Dar es Salaam.

Kabla ya kukabidhi, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) litakutana na uongozi wa Hospitali ya Temeke kupanga maeneo ambayo fedha hizo zitatumika kwenye hospitali hiyo.

Mechi hiyo ya uzinduzi rasmi wa msimu wa 2012/2013 itafanyika Jumanne ya Septemba 11 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.

Viingilio kwenye mchezo huo vitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya bluu na kijani, sh. 10,000 viti vya rangi ya chungwa, sh. 15,000 kwa viti vya VIP C na B wakati VIP A itakuwa sh. 20,000.

WACHEZAJI WAWILI WAOMBEWA ITC URENO

Shirikisho la Mpira wa Miguu la Ureno (FPF) limetuma maombi Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupatia Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa wachezaji wawili waliokuwa wakicheza mpira nchini.

Wachezaji wanaoombewa ITC ni Hamis Thabit Mohamed (19) ambaye klabu yake ya mwisho aliyoichezea nchini ilikuwa African Lyon wakati mwingine ni Abuu Ubwa Zuberi (20) ambaye msimu uliopita alikuwa akiichezea timu ya Yanga.

Kwa mujibu wa FPF, wote wawili wanaoombewa ITC kama wachezaji wa ridhaa (amateur) ili waweze kujiunga na timu ya Atletico Sport Clube ya Ureno ambayo hata hivyo haikuelezwa iko daraja gani nchini humo.

Pia FPF imeombwa kupatiwa hati ya maelezo ya mchezaji (player’s passport) kwa kila mmoja ikiwemo taarifa za ushiriki wao katika mechi rasmi zinazotambuliwa na TFF wakiwa katika klabu zao hizo za zamani.

STARS YAPANGIWA UGANDA CHAN 2014

Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) imepangiwa kucheza na Uganda (The Cranes) katika raundi ya kwanza ya michuano ya kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) zitakazofanyika Afrika Kusini mwaka 2014.

Kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa jana (Septemba 7 mwaka huu) makao makuu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) jijini Cairo, Tanzania imeingia moja kwa moja raundi ya kwanza ambapo itacheza na Uganda.

Mechi ya kwanza itachezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam kati ya Juni 21,22 na 23, 2013 wakati ya marudiano itakuwa Uwanja wa Mandela ulioko Namboole jijini Kampala kati ya Julai 5,6 na 7, 2013.

Nchi 38 zinashiriki katika mechi hizo za mchujo ambapo nyingine zitaanzia raundi ya awali itakayochezwa kati ya Novemba 30 na Desemba 1 na 2 mwaka huu wakati mechi za marudiano zitakuwa kati ya Desemba 14,15 na 16 mwaka huu.

Ratiba imepangwa kwa makundi ya kanda ambapo jumla ya timu 16 ndizo zitakazocheza fainali hizo nchini Afrika Kusini. Kanda hizo ni Kaskazini itakayopeleka timu mbili katika fainali, Magharibi A (timu mbili), Magharibi B (timu tatu), Kati (timu tatu), Kati Mashariki (timu tatu), Kusini (timu tatu akiwemo mwenyeji Afrika Kusini).

Kwa upande wa kanda ya Tanzania (Kati Mashariki), timu zinazoanzia raundi ya awali ni Burundi, Eritrea, Ethiopia na Kenya.

Fainali za Kwanza za CHAN zilifanyika mwaka 2009 nchini Ivory Coast ambapo Tanzania ilishiriki huku Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) ikiibuka bingwa. Fainali za Pili zilichezwa mwaka 2011 nchini Sudan ambapo Tunisia ilitwaa ubingwa. Fainali za Kwanza zilishirikisha timu nane kabla ya kuongezwa hadi 16 za sasa.

Boniface Wambura

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments:

Post a Comment